28/01/2024
*DKT JAFOASISITIZA MATUMIZI YA NISHATI YA GESI KATIKA KULINDA NAKUHIFADHI MAZINGIRA NCHINI.*
KISARAWE PWANI
KAMPUNI ya Oryx Gas Tanzania kwa kushirikiana na Waziri wa Nchi, Ofisi ya Makamu wa Rais, Muungano na Mazingira Dk.Selemani Jafo wamekabidhi mitungi 700 ya gesi pamoja na majiko yake kwa walimu 500 pamoja na Baba na Mama Lishe 200 yenye thamani ya zaidi ya Sh.milioni 50 katika Wilaya ya Kisarawe mkoani Pwani huku kampuni hiyo ikiahidi kufunga mfumo wa gesi katika Shule ya Sekondari Minaki ili waanze kutumia nishati safi ya kupikia badala ya kutumia kuni na mkaa.
Akizungumza wakati wa hafla ya kukabidhi mitungi hiyo kwa walimu wa shule za msingi na sekondari Wilaya ya Kisarawe Mkurugenzi wa Kampuni ya Oryx Gas Tanzania Benoit Araman amesema anamshukuru Waziri Jafo, kwa kumpatia nafasi ya kupeleka nishati safi ya kupikia kwa walimu pamoja na Baba na Mama lishe wilayani Kisarawe.
“Oryx Gas tunaamini kwamba ukipika kwa kutumia gesi, inaleta maendeleo mengi kwa jamii yetu. Kupika kwa gesi ya Oryx ni kulinda mazingira kwa kuacha kukata miti. Zaidi ya yote ni kulinda afya ya wanawake kwa kuwaepusha kuvuta moshi na mvuke unaoathiri mapafu na afya yao unaotokana na kuni na mkaa.
“Wanawake wanatumia muda mchache kupika hivyo wanapata nafasi kufanya shughuli nyingine za maendeleo na kuepuka kugombana na wenza wao kwa kuchelewesha chakula, na wanaume pia watajiongezea marks ukiwazadia wamama mitungi ya gesi.Kwa kutumia gesi ya Oryx, Watoto wanakua na muda mwingi zaidi kusoma na sio kwenda kutafuta kuni.”
Amesisitiza kuwa kuanzia Julai mwaka 2021 wamekuwa mstari wa mbele kutekeleza maelekezo ya Serikali waliyopokea kutoka kwa Rais wa Jamhuri wa Muungano wa Tanzania kuwa ifikapo mwaka 2032 asilimia 80 ya Watanzania wawe wanatumia nishati safi ya kupikia.
Araman amesema kupitia mipango hiyo Oryx Gas inataka kutokomeza matumizi ya nishati chafu ya kuni na mkaa ambayo si tu mbaya kwa afya bali pia ni hatari kwa mazingira yetu huku akitumia nafasi hiyo kueleza pia Oryx Gas inatekeleza juhudi za kueneza matumizi ya nishati safi kwa Watanzania wengi ipasavyo ambayo ni ndoto kubwa ya Rais Mama Samia Suluhu Hassan.